Published at: Thu, Dec 7, 2023 1:51 PM
Kampuni ya Oxford University Press, kupitia mamlaka ya Elimu Tanzania imetoa msaada wa vitabu zaid ya elfu ishirini na nne (24,567) vyenye thamani ya shilingi milioni 100 na moja, laki moja na thelathini na tisa elfu mia tano (TZS 101,1395000) Kwenye shule za msingi 48 za mikoa ya Pwani na Dar es salaam.
Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Mheshimiwa Majdi Hemed Mwanga na Kaimu Mkurugenzi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania Bwana Joel Laurent, wamevipokea vitabu hivyo kwa niaba ya Serikali tarehe 22 April 2015 katika shule ya msingi Majengo iliyopo Wilaya ya Bagamoyo.
Mamlaka ya Elimu Tanzania kwa kushirikiana na maafisa elimu husika kutoka wilaya za mikoa ya Pwani na Dar es salaam wamezichagua shule za msingi arobaini na nane kwakuzingatia uhitaji. Ingawa takribani shule zote zina upungufu wa namna fulani wa vitabu, lakini zipo shule ambazo zina uhitaji Zaidi kuliko nyingine, ndizo zilizopewa kipaumbele.
Kaimu Mkurugenzi mkuu wa TEA, Joel Laurent alisema, “Msaada huo umekuja muda mwafaka kwani serikali imebainisha katika sera mpya ya elimu ya mwaka 2014 kuwa itahakikisha kuwa lugha ya Kiswahili, Kiingereza na nyingine za kigeni zinafundishwa kwa ufasaha na ufanisi katika ngazi zote za elimu na mafunzo nchini ili kuleta ufahamu na umahiri kutokana na umuhimu wa lugha hizo katika masuala ya kitaifa, kikanda na kimataifa”
Naye mkuu wa wilaya Mhe. Mwanga, alisisitiza umuhimu wa matumizi mazuri ya vitabu hivyo ili kukidhi malengo ya msaada na kuongeza maarifa ya lugha ya kiingereza kwa wanafunzi.
Kwa ujumla, kutokana na tathmini ya mwaka 2013, Tanzania ina upungufu mkubwa wa vitabu vya kiada.
Naye Meneja mkuu wa Oxford University Press Bibi Fatma Shangazi alisema, “Haitoshi tu kuyabainisha matatizo yaliyopo katika shule zetu, au katika sekta ya elimu kwa ujumla. Kinachohitajika zaidi ni kuchukua hatua katika kutatua matatizo hayo”
Mamlaka ya Elimu Tanzania, kwa niaba ya serikali na Wizara ya Elimu na Mafunzo, inatoa shukrani za dhati kwa makampuni haya yaliyotoa ufadhili huu. Pia Mamlaka ya Elimu Tanzania inatoa wito kwa Makampuni, Mashirika ya umma na binafsi, asasi zote na watu binafsi kuendelea kujitolea kufadhili miradi ya elimu na kutoa misaada pale inapo bidi katika kuhakikisha upatikanaji wa elimu bora na usawa na kwa wote